Aliyekuwa Mwenyekiti wa CHADEMA wilaya ya Makete Shaaban Mkakanze.
Na Edwin Moshi, Makete
Hatua hiyo imefikiwa baada ya mkutano wa wanachama uliofanyika jumamosi machi 8, mwaka huu kwa pamoja kuazimia kuung’oa madarakani uongozi uliokuwepo baada ya kujadiliana kwa kina katika mkutano huo.
Miongoni mwa viongozi waliong’olewa ni pamoja na mwenyekiti wa chama hicho wilaya ya Makete Bw. Sahaaban Mkakanze na katibu wake pamoja na uongozi mzima uliokuwa ukiongoza chama hicho wilaya
Mkutano huo ambao pia uliowashirikisha viongozi wa chadema mkoa wa Njombe akiwemo mwenyekiti Bw. Lulandala, ulibaini kuwa kasi ya kukua kwa chama hicho wilayani Makete ni ndogo ukilinganisha na maeneo mengine licha ya jitihada zinazofanywa na ndiyo maana wakaona wabadilishe uongozi.
Katika mkutano huo waliazimia kuchagua uongozi wa muda ambao umepewa miezi miwili ya matazamio kuhakikisha wanakiimarisha chama katika kata zote za wilaya ya Makete ikiwemo kuunda uongozi wa kila kata ambao unaweza kufanya kazi kama inavyotakiwa
Viongozi wa wa muda waliochaguliwa kushikilia chama hicho ngazi ya wilaya kwa muda ni Bw. Ibrahim Ngogo ambaye ni mwenyekiti, Bw. Ilomo ambaye ni katibu na Bw. Stephano Kasanga ambaye ni katibu mwenezi
Mkutano huo umewapa miezi miwili ya kukiimarisha chama kabla ya kuitishwa mkutano mwingine ambao utakuwa wa uchaguzi wa wanachama kuwachagua viongozi wa wilaya wa kukiongoza chama hicho.

